Ukurasa wa mbele
Soma barua Yahoo
Soma barua Hotmail

 


 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 



TV ya INJILI
Kwenye Internet
-
WWW.GOSPELGTV.COM

Tel. 254722602445 E-mail:
munishi@munishi.com or info@munishi.com

TELKOMKenya Wazinduka usingizini

Walizoea ukiritimba wa kuwa peke yao, ndiyo maana kupata simu enzi zao ungebidi uwaonyeshe vitu vingi sana.Kuanzia kitambulisho, cheti cha kuzaliwa na PIN namba. Tena ungejaza fomu inayokutaka useme kama una kazi au la. Na kama unayo, useme ni kazi gani na kwa nini ufanye kazi hiyo.Ukifikiri vikwazo vya kupata simu vitaishia hapo, wanakuambia uwaletee picha tatu saizi ya paspoti, na tena ziwekwe saini ya wakili wa serikali nyuma kuthibitisha kama kweli ni wewe. Hata kama una alama nyingi usoni kama mimi, bado wangesisitiza uwaletee picha tatu. Na hiyo ni fomu ya ombi la kuwekewa simu nyumbani au ofisini.Iliwabidi wengi wayapitie mateso yote hayo ili tu siku moja wajikute wanaweza kuwasiliana kutumia kifaa kiitwacho simu, au TELLEPHONE kama wanavyoziita wale waliotutawala miaka arobaini iliyopita. Waliokuwa na uwezo walikwepa vizingiti vyote hivyo kwa kuwauliza wafanyikazi wa Posta wawaambie ni pesa ngapi wangetaka ili mtu apate simu bila kuruka virunzi vyote hivyo. Hapo RUSHWA ikaota mizizi katika shirika hilo kwa kiwango cha kutisha. Wengi wakati huo walikata tamaa na hawakujaribu kukanyaga ofisi za TELKOM wakati huo walkiitwa Kenya Posta.

Nani Zaidi?


Kama wasemavyo waswahili "Kilicho na mwanzo hakikosi mwisho wake, Hakuna mtu aliyetarajia kwamba maringo na makidai ya shirika la Posta yangefikia kikomo siku moja. Hao hao waswahili wana msemo kwamba "Upole wa paka usikudanganye umpige bila kumwachia mwanya wa kutorokea. Ukifanya hivyo, macho yako yatakuwa ndiyo mwanya.Ataruka kima usawa na macho yako, na kingine utakachokiona ni giza totoro baada ya macho yako kukumbana na kucha kali za paka." TELKOM hawakuomba iwe hivyo kwao, Lakini sijui SAFARIOM na CELTEL walitokea wapi, wakafanya kile ambacho paka angefanya. Waliruka kima usawa wa macho ya TELKOM, Wakawamwagia vumbi zito, kiasi kwamba hawakuyaamini macho yao kibiashara kwamba yamezimwa. Walijikuta pale ambapo wananchi walikuwa kila siku wanapozuru ofisi za TELKOM. Kuomba kwa magoti uwekewe simu, ikawa sasa ni zamu yao kuwaomba wateja kwa magoti wakubali kuwekewa simu.

Hata hivyo walisahau kwamba aliyekwisha umwa na nyoka, huogopa kusogelea hata kijiti kinachofanana na nyoka. Nilijikuta nikiogopa hivyo mjini Nairobi hivi majuzi wakati nilipowakuta TELKOM wakiwa wameweka kibanda nje na wanawabembeleza wateja wakubali kuunganishwa katika simu zao ambazo sasa ni bila waya. Yaani ni ile ile simu iliyokuwa inawekwa kwako kutumia waya mrefu kutoka mbali, sasa unaipata kwa kununua kadi simu mfano wa zile za simu za mikononi. Na pia kifaa utakachoweka smu kadi hiyo, kinafanana kabisa na kile wanachotumia wakali wao kina SAFARICOM na CELTEL. Tofauti ni masafa. Usijali kama ulikuwa unajua kwamba simu za mikononi tunazotumia hupeperusha mawasiliano zikitumia masafa ya GSM. La muhimu kwa wengi ni simu iongee, na wao wawasiliane.Hayo ya GSM na CDMA hayawahusu wengi. Wala hawapotezi muda kutaka kujua. Hata mimi ni vivyo hivyo, lakini nilijikuta nikikaa chini nipewe somo na wana TELKOM.

Kwanza walinikaribisha vizuri sana katika kibanda chao. Hiyo ikanitia mashaka kwa sababu ninawajua tangu enzi zao za KENYA POSTA.. "Karibu sana tuna tekniloji mpya hapa ambayo inakuwezesha kuwa na Land Line MObile." Nilijivuta ndani sawa sawa niweze kusikia jipya." Unaona kwamba sisi TELKOM tumeamua kuwakomboa kutoka utumwa wa SAFARIKOM na CELTEL. Ukiwa na shilingi elfu moja tunakuuzia simu kadi. Ukitaka kuunganishwa lazima ununue simu ya mkononi lakini inayotumia masafa ya CDMA." Alisema dada mmoja mama wa makamo kidogo, jambo lililoashiria kwamba amekuwepo tangu enzi zile.Niliduwaa kidogo baada ya kutajiwa CDMA, lakini nikajikaza kisabuni na kuuliza nifahamishwe zaidi.Waswahili husema kuuliza siyo ujinga. Ndipo nilipopewa somo kwamba CDMA ni teknoloji ambayo imekuwepo zaidi ya miaka mia, na imekuwa ikitumika na majeshi hasa ya Amerika.Sasa huendaikawa majeshi hayo yamepata teknolojia mpya ndiyo maana wameamua kuacha CDMA itumike kwa mawasiliano ya kibiashara. Nikakumbuka stori kama hiyo nilipokuwa nikinunua simu yangu ya mkononi ya kwanza.Tofauti ya ile ya kwanza ni GSM.



Sasa kabla sijakuchanganya na hizi lugha za tekniko, hebu nikuambie nilivyoambiwa yaishe. Waliniambia kwamba ninaweza kununua simu ya CDMA kwa Kshs. 7,000 na nitaweza kuitumia simu yangu kama vile ningetumia simu ya kawaida ya LAND LINE. Bei ni chini ukilinganisha na SAFARICOM na wenzao KENCEL. Tena walisema ukiwa na simu hiyo ya CDMA itakuwezesha kuingia kwenye mtandao wa kompyuta duniani yaani INTERNET kwa bei ile ile ya kupiga simu 'LOKOL.' Nilijikuta ninashawishika, kwani mimi mara nyingi hupenda kuingia kwenye mtandao kuandika story kama hii unayoisoma. Mara nyingi huandika usiku baada ya kazi nyingine za mchana, na ingekuwa vizuri kwangu kama ningeweza kuingia kwenye mtandao wakati wowote na kwa bei nafuu. Kwa hilo tu kwamba nitaingia kwenye INTERNET na nitalipa dakika za simu pekee bila kulipia Internet, tena kwa bei ya 'LOKOL', niliona kwamba TELKOM wako sawa kibei kuliko makampuni mengine.Tena wanadai kwamba ukijiunga kwenye mtandao kutumia sava zao, utapata kile unachokitaka kwenye Internet upesi kwani tovuti yao ina mbio kali.Hilo sikumeza kabisa hapo kwa hapo, bali niliwaambia nikiweza kuingia kwenye mtandao na nione kweli mbio wanayoisema iko, hapo nitawaamini. Nilinunua simu kadi yao Kshs.1,000 huku nikilalamika kwamba kama kweli wamekuja kututoa utumwani, basi hata bei ya simu kadi bado iko juu. Nilipotaka waniuzie pamoja na simu, walinielekeza kwa wauzaji wa simu. Hapo niliona ujanja wa TELKOM. Hawataki kuhusika na uuzaji wa simu ndiyo maana wamewapa tenda kampuni binafsi kufanya kazi hiyo.

Hapa ni mtambo wa CDMA ambao TELKOM wanasema utayabadili maisha ya Wakenya. Kutumia simu hii kutamuwezesha mteja kupiga simu kwa bei ya land line japo ni Mobile. Tena kuunganishwa kwenye mitambo ya INTERNET haijawahi kuwa rahisi hivi. Ukiwa CDMA kompyuta yako inaunganishwa na zile nyingine ulimwenguni kote kutumia mtandao wa INTERNET.

Nikanunua simu ya CDMA Nokia 6602 kwa bei ya Kshs.7,100 Bado hata hapo nililalamika kwani simu ya kiwango hicho lakini ni GSM bei yake ni ndogo mara mbili ya hiyo ya CDMA. Hilo pia niliwaambia. Nikawalipa pesa. Nikapewa risiti ya simu. Kabla nipewe risiti ya simu kadi, wakaleta fomu ya kujaza. Nilipoitupia macho nikakuta ina karibia zile za enzi zile japo hii haitaki picha tatu. Lakini kuna sehemu inayokutaka ujaze ulizaliwa lini. Hapo niliona nisikae kimya. Niliwauliza hii wanayoiita teknoloji mpya inawabagua watu waliokula chumvi nyingi kama mimi? Na ni kwa nini watake kujua miaka yangu? CDMA na umri wa mtu vinaingiliana wapi? Nikajua bado yale ya enzi zile hayajawatoka kabisa. Nikajipa moyo na nikajaza miaka yangu na wakanipa simu kadi. Nilipoiweka kwenye CDMA yangu na kuona kwamba ninaweza kuwasiliana na mtu kwa land line Mobile yangu, nilifurahi utadhani nilipewa zawadi. Lakini ukilinganisha na mateso ambayo mtu alipaswa kuyapitia ndipo apate simu enzi zile, siyo ajabu ukimuona Munishi akicheka mpaka jino la mwisho kuonekana. Ni ajabu kwake kuona wabembelezwa wakibembeleza.Tena ni ajabu kuona kwamba simu ambayo ungeweza kuomba na ikachukua mwaka na wakati mwingine hata miaka miwili bila kupata, sasa unanunua na unakwenda ukiongea. Furaha yangu haikudumu sana kwani kufika nyumbani simu yangu ya CDMA ikaleta kasheshe. Nikipiga, niliyemwita namsikia lakini yeye hanisikii. Nilipowaita watu watatu na tatizo likawa ni hilo, nilijua nimeliwa.Kuangalia risiti nikakuta nambari ya simu ya wenye kampuni ya uuzaji wa CDMA. Nilipojitambulisha, na hapo nilikuwa natumia GSM ya SAFARICOM, Nikawaeleza tatizo langu na CDMA. Wakawa watu wazuri sana. Walinitaka nirudi pale pale niliponunua simu ili waikague na kisha wanipe nyingine. Kweli kesho yake nilipofika waliikagua simu na wakanipa nyingine bila kulipa chochote. Nilipowauliza jinsi ya kuiunganisha CDMA na kompyuta yangu ili niweze kuingia kwenye mtandao wa INTERNET waliniambia inatakiwa kebo maalum ambayo hawana.Tena kutaitajika 'SOFT WEAR' ambayo hawana. Tena kutahitajika kuinstol hiyo soft wear pamoja na kukomfiga, ambayo pia hawajui kuifanya.




Hapo ndipo niliposema Mungu nisaidie. Ikiwa wenye CDMA hawajui inafanywaje, mimi nitafanikiwa kweli? Nilikumbuka msemo ule ule. "Aulizaye siyo mjinga." Nilianza kuwauliza marafiki wenye ujuzi na kompyuta kuliko mimi, na mmoja wao akaniambia hiyo ni rahisi sana. Alijigamba kwamba makampuni yote yanayojihusisha na CDMA bado jinsi ya kuunganisha simu ndogo za CDMA na kompyuta inawapiga chenga. Na kwa sababu wao siyo kama Munishi, wanaogopa kuuliza. Na hata wakijua unajua, hawataki kujiaibisha waonekane kampuni kubwa kama hiyo inaingizwa mjini na kitu kidogo kama "DRIVER za kuifanya simu ya CDMA iwe 'MODERM." Baada ya kusema hayo, nawapongeza TELKOM kwa kuzinduka usingizini. Lakini itawabidi wawe makini kwani kibarua kilicho mbele yao ni kigumu. SAFARICOM na CELTEL wamekita mizizi kiasi kwamba wakisikia TELKOM wameamka, hawatasita kuteremsha bei na kuifanya huduma ya INTERNET kuwa rahisi kupitia masafa ya GSM. Naomba Mungu anipe uhai ili nione na hayo pia.

Tofauti na Enzi zile za kuletewa bili za uongo, sasa unanunua kadi ya kiwango unachopenda. Ukitumia salio liishe, huwezi kuwasiliana tena.Ila bado kuna wasiwasi kama watakuwa waaminifu walipishe kama wanavyosema na siyo kama wapendavyo.Ukiweka pesa kwenye akaunti yako, sijui utajuaje umetumia kiasi gani kwani TELKOM bado hawatumi ujumbe mfupi kuonyesha salio.Badala yake ujumbe wa sauti inayokoseakosea hukwambia salio lako.Wengi wanasema ingekuwa bora wawe na uwazi. Hasa mtu anapojiunga kwenye internet ni vigumu kujua ni wakati gani wanapoanza kukulipisha. Je ni wakati tayari ukurasa wa Internet umefunguka? au hata wakati wa kujaribu kuunganishwa unalipishwa? Niliweka mia nne na ziliisha kabla sijafanikiwa kuingia kwenye internet. Sikujua ziliishia wapi. Hapo napo kuna kibarua upande wa TELKOM ili warudishe imani kwa wateja. Huku hayo yakijiri, Bado kuna makampuni mawili yanayoshindana na TELKOM katika masafa ya CDMA. Kampuni kama FLASHCOM na POPOTE wanawapa TELKOM kichefuchefu na kukosa usingizi. Lakini kwetu wateja ni furaha. Kwani wanaposhindana, bei zitakuja chini na itakuwa rahisi kuwasiliana.

Hawa ni FLASHKOM. Pia wao hutumia CDMA. Ila kimasafa wanatofautiana na TELKOM ndiyo maana hata simu zao zinatofautiana. Lakini tuwape muda.Sitoshangaa kuona sokoni simu moja inayotumia masafa yote. Yaani GSM na CDMA zote pamoja kwenye simu moja.Tayari ukienda River Road kuna wataalam wanaoweza kuifanya simu yako ya GSM iweze kufanya kazi kama CDMA. Tatizo bado ni bei zao. Ukiwasikiliza utakuta kuna ujanja ujanja ndani. Watakwambia ni Internet inaanzia Kshs.2000 kwa mwezi. Ukisisimka useme haya chukueni elfu mbili wanakuambia ngoja kwanza. Hiyo haitoshi. Lazima ulipe deposit ya kiwango kama hicho. Tumbo linaanza kuingia baridi. Na kwa sababu anayekueleza hivyo ni msichana mrembo aliyesomea kazi ya kuuza kila kitu, unaona usimkosee kiumbe kama huyo. Unasema haya basi nimeongeza elfu mbili ziwe nne. Unauliza huku sauti ikianza kukwaruzana kwani haukuwa tayari kutumia kiwango hicho cha pesa. Je nikilipa hiyo nitapata huduma ya Internet kwa mwezi mzima? Unaambiwa ndiyo lakini..... Jasho jembamba linaanza kukutoka ukitaka kusikia lakini ni ya nini tena Yarabi? Wanakuambia ukilipa hizo pesa utaweza kuingia kwenye mtandao masaa ya usiku pekee. Mchana wote ukitaka kuingia kwenye Internet, ni lazima ulipie masaa mchana. Unaanza kusikia kizunguzungu. Unauliza. Nitalipaje? Unaambiwa utaletewa bill baada ya kujaza fomu na kusaini mkataba na FLASHCOM. Machoni kweli unaona vitu kama vinaflashflash. Kama akili yako inafanya kazi haraka kama ya sungura, unasema sitaki. Rudisheni pesa zangu. Mbona kuna ujanja ujanja mwingi? Si muifanye rahisi tu? Mbona isiwe bei moja kwa wote? Yaani wale wanaotaka kununua kadi za kukwaruza wanunue za kiwango wanachoweza, Na wale wasiotaka usumbufu wanunue kiwango cha mwezi mzima? Hapo unatakiwa uwazi tu. Kwamba Internet kwa mwezi ni shilingi kadhaa. Lakini sharti liwe ni kulipa hizo pesa kabla hujaanza kutumia. Hiyo itaokoa mambo mengi ya kutuma na kupokea bill ambazo lazima kuwe na watu wa kuthibitisha ni za kweli. Japo hata kununua jumla kuna hatari zake, lakini siku hizi kuna programu zinazoweza kuonyesha mtumiaji wa simu aliitumia vipi.Hiyo ingetufanya sisi kina yahe, tusiotaka kutumia pesa zote kwa simu kujipanga. Lakini kwa mtindo huu wa ujanja ujanja mwingi wa wale waliosomea kuuza, wengi bado tutakimbilia kwenye vibanda vya Internet ambayo vinatoza senti hamsini za Kenya kwa dakika moja. Yaani ukiwa na senti hamsini unaweza kuingia kwenye mtandao Kenya. Hii ni tofauti kabisa na vibanda kama hivyo nchini Tanzania. Huko wanakulazimisha kukaa nusu saa hata kama shughuli yako itakuwa imemalizika baada ya dakika tano. Wanakupa kibarua kigumu cha kuamua kusuka au kunyoa. Yaani ukimaliza kabla ya nusu saa uwalipe nusu saa na uende.Au ukae hapo ukiiangalia kompyuta yao kama huna la ziada.Isitoshe makampuni ya simu Tanzania yanalipisha kwa dola na siyo shilingi za Tanzania. Kisa wanasema shilingi ya Tanzania imeshuka thamani mpaka kompyuta za makampuni ya simu zinakataa kuwalipisha watu kutumia shilingi. Hebu nirudi Kenya kwa FASHCOM. Ukishanunua kadi za kukwaruza na uweke kwenye simu yako bado kuna kibarua cha kuwatafuta wajanja wa River Road wakuuzie kebo itakayoiunganisha simu yako na kompyuta yako ili uweze kuingia kwenye mtandao. Usiniulize kwa nini Kampuni inayojigamba kuwa ya kwanza kuleta CDMA Kenya haina wataalam pamoja na kebo za kuwaunganisha wateja. Hiyo inashangaza kwani wengi tungetegemea kupata usaidizi wote kuhusu CDMA hapo FLASHCOM. Kwamba ni lazima uupate kwingineko hiyo inafanya mambo kuwa magumu. Mfano ni wakati umetafuta kila kitu na hatimaye kompyuta yako ikaweza kuonana na simu kisha kujiunga kwenye mtandao. Hapo unatakiwa uombe Mungu chochote kisiende mrama. Endapo mawasiliano na mtandao yatakatika ghafla utashindwa nani wa kuuliza. Yule wa River Road, au Wanaojiita mainjinia wa Flashcom? Yaliponikuta hayo, niliamua kwanza nimuulize mtaalamu wangu. Kwamba aliweza kuifanya simu yangu ionane na kompyuta yangu kisha nikaweza kuunganishwa kwenye mtandao kupitia FLASHKOM, kwangu huyo ndiye mtaalam wa kweli. Nilimuuliza vipi naingia kwenye mtandao na sioni ukurasa ukifunguka? aliniuliza ninapata ujumbe gani kwenye ukurasa uliokataa. Nikamwambia inasema ukurasa hauwezifunguka. Mara moja akajua tatizo ni Flashcom ndio hawako kwenye mtandao wakati huo. Sababu inaweza kuwa watoa mtandao wamekatiwa mtandao kwa kukosa kuwalipa wanaowapa huduma hiyo, au iwe ni hitilafu za mitambo. Nilipojaribu kuwapigia FLASHCOM nijue kulikoni, wao walijaribu kuuzunguka mbuyu badala ya kusema kweli hawako kwenye mtandao. Watakwambia nenda kwenye internet OpKwa FLASHCOM ni mwanzo mzuri na tunawatakia kila la kheri.

Huu ndio mtambo wa CDMA wanaotumia kampuni ya FLASHKOM. Tofauti na ule wa TELKOM, huu kidogo bei yake iko chini. Ukiwa na Kshs. 4500 unaweza kupata simu ya CDMA inayoweza kufanya na mitambo ya FLASHCOM. Ila sim card za Flashcom ni Kshs.1,500. Ila kuna tatizo linalowakumba wote. Network zao bado ziko Nairobi pekee. Ukitoka nje ya Nairobi kidogo tuseme uwe Ngong, Network inaanza kupotea. Mwenyewe nilinunua Land line Mobile ili niweze kuingia kwenye internet usiku baada ya kazi, lakini kwa mshangao nimekuta kwamba sehemu ninayoishi ya Ngong bado masafa yao ya CDMA hayafiki sawasawa. Bado wanahitajika kuvuta soksi zao ili waweze kutangaza kwamba wamekuja kututoa kwenye utumwa wa SAFARICOM na CELTEL. Vinginevyo Safaricom wakipunguza bei kidogo, na wawaruhusu watu kuingia kwenye mtandao kwa bei nafuu, wengi watachagua kubakia utumwani, kwani waliuzwa huko na hao hao wanaojaribu kuwatoa huko.


Nao Safaricom ni kama wanachunguza kila hatua wanayochukua kina TELKOM na FLASHCOM ili waje na sunami ya bei itakayowafanya wapinzani waone vumbi mbele yao. Tunasubiri tuone Wakenya wakielekea mahali pa kupiga simu bure kama siyo kutuma jumbe fupi bure, au zote pamoja.


Celtel wamekazana kuunganisha mtandao Afrika ya mashariki. Wanachosahau ni kwamba watumiaji wa simu za mikononi Uganda na Tanzania pamoja hawafikii idadi ya watumiaji simu hizo Kenya. Sababu kubwa ikiwa bei za simu Uganda na Tanzania ni ghali ikilinganishwa na Kenya. Tanzania kuongezea salio lako ni lazima ufanye hivyo kwa dola na siyo shilingi za Tanzania. Inasemekana makampuni ya simu yalidaiwa rushwa ya kiwango cha juu na watawala Tanzania, na mzigo huo wanawabebesha watanzania. Usijali kwamba Tanzania na Uganda ndio walioanza kuwa na simu za mkononi, lakini msemo "Kutangulia siyo kufika" utamaanisha sana hasa kwa Tanzania.

Badala Celtel watumie mabilioni kuunganisha mtandao, wangepunguza bei zao ziwe chini ya zile za Safaricom na watu wote wangehamia huko na na kupiga simu Afrika ya mashariki ingekuwa rahisi. Endapo bei Celtel zitabaki kama zilivyo, basi wapinzani wao wa jadi Safaricom wataendelea kutamba sana Kenya ambako soko la simu ni kubwa kuliko masoko mawili ya Uganda na Tanzania. Haiingii akilini kwamba Celtel wanaacha soko kubwa kuliendea soko dogo tena kwa kutumia mabilioni. Kwa nini mabilioni hayo yasingetumika kuwafanya wateja wa Celtel kupiga simu bure kwa miezi miwili ili kuvuta wateja zaidi?

Ukweli wa mambo ni kwamba Celtel bei zao ni juu ukilinganisha na Safaricom. Tena wasisahau kwamba Flashcom wako uwanjani na bei zao ni chini kuliko wote. Kama wangekuwa na mtandao unaopita Nairobi, mambo yao yangekuwa mazuri zaidi. Lakini hata soko la Nairobi pekee linaweza kuwafanya Flashcom waanze kugonga chati. Tunaomba Mungu amguse Kibaki ili kabla hajamaliza muda wake aunde serikali ya Uganda Made in Kenya, Halafu ifuatie serikali ya Tanzania Made in Kenya, halafu roho ya Afrika ya mashariki itakuwa imeshika joto linalostahili.

Msisahau kwamba yote hayo Kibaki anayaweza kwani aliunda serikali ya Somalia Made in Kenya na inafanya kazi mpaka sasa. Hata Sudan aliwaundia Serikali. Msishangae kumuona Munishi siku moja akiingia kwenye Benzi na serikali yake wakielekea Tanzania kupitia Namanga. Wakati huo makampuni ya simu Tanzania yatapunguza bei zao ziwe karibu na bure kwani serikali ya Munishi haitakuwa ikichukua Rushwa toka kwa makampuni hayo kama serikali ya Kikwete inavyofanya. Kumbe wanasiasa ndio wanaofanya bei za simu kuwa ghali?

 

 
| http://munishi.com |